Wednesday 5 June 2013

MPIGA DEBE WA DALADALA AMWAGA NGELI NA KUWASHANGAZA WENGI………

 





Leo asubuhi nimekutana na kituko cha mwaka, naomba nikiri kwamba hata mimi nilikuwa ni mjinga kwani sikutarajia kwamba jambo hilo nililolishuhudia linawezekana. Naomba nikiri kuwa hata mie nilikuwa nawapa watu hawa mtazamo tofauti kabisa nikidhani labda mie ni mjanja kuliko wao, lakini hili nililolishuhudia asubuhi ya leo, nimenifunza jambo moja muhimu sana maishani, kwamba kamwe usimhukumu mtu kutokana na muonekano wake.

Ilikuwa ni majira ya saa kumi na mbili alfajiri, niko maeneo ya Msasani, nikisubiri daladala la kuelekea Kariakoo, mara likaja basi moja hivi aina ya Toyota Coster. Kama kawaida abiria wakiwemo wanafunzi tulilikimbilia na kuanza kugombea kupanda kila mtu akijaribu kuwahi kiti. Japokuwa hatukuwa wengi, lakini nilishangazwa na jinsi abiria walivyokuwa wakigombea kupanda utadhani watakosa nafasi ya kukaa. Lakini cha kushangaza ni kwamba vurugu zote zile ilikuwa ni ili kuwahi viti vya Dirishani!

Pale mlangoni alisimama mpiga debe mmoja ambapo kwa hapa Dar hujulikana kama Mateja, yaani watumia madawa ya kulevya, ambaye alikuwa amevaa nguo kuu kuu na zilikuwa chafu ajabu. Alikuwa pale mlangoni kuzuia wanafunzi wasipande. Kwa hapa Dar ni jambo la kawaida wanafunzi kuzuiwa wasipande kwenye basi na abiria wakabaki wakiangalia tu, kama vile haiwahusu. Kule Arusha mambo ni tofauti kidogo, wanafunzi huwa hawaachwi, tena kama hajavuka barabara, hasa watoto wadogo, kondakta anamfuata na kumvusha ili apande kwenye basi, kwa kweli nilishangazwa na ustaarabu wa makondakta wa daladala za Arusha.

Baada ya abiria wote kupanda, yule mpiga debe aliwaambia wale wanafunzi kuwa atachukua wanafunzi sita tu, wengine waende kwenye mabasi mengine. Pale chini kulikuwa na wanafunzi zaidi ya kumi na tano hivi na wote walionekana wakitaka kupanda kwenye hilo basi ili kuwahi shule. Yule kijana mpiga debe aliongea kwa usataarabu akiwaelewesha wale wanafunzi, akiwaambia kuwa hata yeye anajua adha ya usafiri kwa wanafunzi lakini ile gari ina Hesabu, yaani wanatakiwa wafikishe kiwango fulani cha hela kwa mwenye gari na wao wabaki na chochote, na kwa kuzingatia kuwa leo ni Jumamosi, ni ngumu sana kupata hesabu ya tajiri.

Lakini kulitokea kutoelewana kati ya wale wanafunzi na yule mpiga debe, wanafunzi walimjia juu wakimwambia aache siasa, wao wanataka kuwahi shule na hawahitaji Lecture pale. Kulitokea kutoelewana, lakini yule mpiga debe alisisitiza msimamo wake wakutaka wapande wanafunzi sita tu. Ni kweli walipopanda wanafunzi sita, aliwazuia wengine wasipande na kuruhusu dereva aondoe gari. Baadhi ya wanafunzi walioachwa pale chini walilazimisha kuning’inia mlangoni, lakini yule mpiga debe aliendelea kuwazuia huku gari likianza kuondoka mdogo mdogo..

Wakati zogo kati ya wanafunzi na yule mpiga debe likiendelea, ghafla akaibuka abiria mmoja, akaanza kumfokea yule mpiga debe, akimuonya kwamba kama hatawaruhusu wale wanafunzi wapande basi atalipeleka basi lile Polisi, yule Mpiga debe hakumjibu alikuwa akiendelea kuzozana na wanafunzi.

Yule abiria alianza kumtolea yule mpiga debe maneno ya kashfa huku akimtisha kuwa atampiga. Basi liliondoka na baadhi ya wanafunzi waliachwa pale kituoni, ndipo yule mpiga debe akamgeukia yule abiria na kumuuliza kisa cha kumkashifu wakati yuko kazini.

Yule abiria akawa kama amechokozwa, alimshambulia yule mpiga debe kwa maneno makali na kumkashifu kuwa hajasoma na ni mvuta unga tu na kibaka wa mtaani.

Yule mpiga debe akamwambia, ni kweli hajasoma, kwa sababu ingekuwa ni jambo la kustaajabisha kukuta mpiga debe msomi, hata hivyo hakuishia hapo, akamtupia swali yule abiria………

"inaonekana mwenzangu umesoma sana eh!….. hivi una degree ngapi mpaka sasa, au una masters?” Yule abiria aliendelea kumtolea maneno ya kashfa yule mpiga debe huku akisisitiza kuwa hajasoma na ni mjinga tu.

Yule Mpiga debe akaonekana kukerwa na yale maneno kutoka kwa abiria mkorofi, akamgeukia na kumwambia, kwa kiingereza, ngoja nimnukuu hapa……..

“Listen my friend, don’t judge me because of what I am doing, I have good education background than you. To be a Daladala tout does not justify that I am ignorant. For your information, I am educated enough to work for a white-collar job. I am here because of frustration, after being fired from my job; I had a nice job with a lot of benefits and privileges, I am not a fool ok!”

Wakati anamwaga kiingereza, kwanza abiria walishikwa na butwaa, na baadae wakaanza kumshangilia wakiwemo wale wanafunzi waliokuwa wakitetewa na yule abiria mkorofi. Hata hivyo yule abiria aliposikia jamaa anamwaga kiingeza, alikaa kimya asiamini masikio yake,hakujibu kitu.

Abiria waliendelea kumchagiza mpiga debe aendelee kutoa dozi kwa mshkaji, na yeye ili kupata ujiko zaidi akaendelea kumwaga ma-vitu, palikuwa ni patamu hapo…….

“You know sometimes people think all daldala touts are drug users and they are not educated ……..… No, you are totally wrong my friend, for this job I am earning more than enough, I can make your salary which you get from you Boss Indians for 10 days. Although I have been fired but I decided to work as a daladala touts rather than stealing someone’s money.”

Kisha akaendelea…..

“Why you are quiet, talk now Mr. Educated” ………… “You see,” akatugeukia sisi abiria na kutuambia ……….. “Mr. Educated have failed to speak even two English words”

Jamaa akajikakamua na kumjibu,

“Hebu ondoka na kiingereza chako cha kuombea maji, mwenyewe unajiona umeongea kiingereza hapo, hamna kitu,unachapia tu”

Mpiga debe hakumkawiza akamjibu…….

“Ok, my English is just for begging water, where is yours, if you can speak only two English words, I will give you ten thousand, right now, in front of passengers, I am not joking”

Yule mpiga debe akatoa elfu kumi na kumpa abiria mwingine aishike, ili kuthibitisha kuwa hatanii. Kumbe jamaa alikuwa ni mweupe, hajui Ngeli, yaani ilikuwa ni aibu, karibu abiria wote wakawa wana mzodoa kwa maneno ya kejeli.

Tulipofika kituo cha Namanga jamaa akashuka kwa aibu na ninadhani alikuwa hajafika safari yake, naona alishuka ili kujisitiri na aibu iliyomkumba mle ndani ya basi.

Nakwambia ilikuwa ni gumzo ndani ya basi lile kila mtu akisema lake wapo waliosema kuwa yule mpiga debe ni mpelelezi wa Polisi, wapo waliosema ni shushushu yaani anafanya kazi usalama wa Taifa. Na hilo ndilo tatizo tulilonalo Watanzania, yaani mtu akijibainisha tofauti na muonekano wake basi ataitwa shushushu…….. Basi na yule mpiga debe akapewa cheo cha ushushushu pale pale, kisa kaongea Kiingereza, kuna wengine walisema sio Mtanzania bali ni Mkenya, kwa kuwa hakuna Mtanzania anayejua Kiingereza kama vile halafu afanye kazi ya kupiga debe, ili mradi kila mtu alisema lake.

Tulifika Kariakoo kilamtu akashika hamsini zake, nimerejea nyumbani jioni hii nikaona niwashirikishe wasomaji wangu

No comments: